Tuesday, December 13, 2016

“Tusheherekee Maulid ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) kwa kupambika na Huruma yake” Sheikh Jalala

                             

                                            TAARIFA KWA UMMA
Ndugu zangu Waislam wenzangu Asalam Alaykum Warahmatullah Wabarakatu,Amani ya Mwenyezimungu iwe kwenu wote. Napenda kwanza niwape hongera kwa waisla wote watanzania kwa tukio hili la kukumbuka kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w), napenda niwape Hongera kwa sababu ya tukio hili kubwa la kuzaliwa kiongozi huyu.
Kama ambayo nawapa hongera Watanzania wote Waislam na wasiokuwa waislam kwa kushirikiana na watanzania wenzao katika tukio hili la Maulid, katika tukio hili la kuzaliwa Mtume wa Huruma, Mtume wa Upendo, mtume wa Mapenzi, Mtume wa Maelewano, Mtume Muhammad (s.a.w.w).
Katika siku hii ya Maulid na katika kuadhimisha kuzaliwa kwa Mtume huyu napenda kuzungumza jambo moja ambalo ni nzito na la muhimu, na sisi kama watanzania wote kwa ujumla Waislam na wasiokuwa waislam tunalihitajia tukio hilo, au tunayahitajia maelezo hayo yanayohusiana na Mtume wetu Mtume Muhammad (s.a.w.w).
Tukio hili napenda nimesome Mtume kwenye upande wa kazi moja kubwa ambayo sisi kama watanzania tunahitajia nayo ni kazi ya Kuwaunganisha watu,Moja ya kazi kubwa muhimu ambayo mtume huyu tunaemkumbuka Maulid na kuzaliwa kwake leo,moja ya kazi kubwa nyeti na muhimu aliyoifanya ilikuwa ni kuwaunganisha watu.
 
Hawa ni baadhi ya waandishi wa habari upande wa Television wakiwa makini kumsikiliza Kiongozi Mkuu wa Waislam Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala.
Mtume Muhammad (s.a.w.w) yeye sambamba na mitume wengine wote waliopita,moja ya kazi yao kubwa ilikuwa ni “Tauhidil Kalima” ni Tauhidil Umma” ilikuwa ni kuwaunganisha watu, kwanzia Mtume Adam (a.s) mpaka kufikia Mtume Ibrahim (a.s), mpaka kufikia Mtume Mussa (a.s), Mpaka kufikia Mtume Issa / Yeu(a.s) na hatimae kufikia kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w), hao wote moja ya mafunzo yao muhimu na makubwa ilikuwa ni kuwafanya watu wawe kitu kimoja.

Hakuna Mtume aliekuja kuja kufundisha mafundisho ya kuwatenga watu, hakuna mtume wa Mungu aliyekuja kuwafunza watu kutengana, bali watu wote walikuja kuwaunganisha watu kuwa kitu kimoja.Siku hii ambayo leo tunakumbuka Mazazi ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) naamimi ya kwamba darasa hili la Umoja aliyoifunza Mtume Muhammad (s.a.w.w), aliyoifunza Nabii Issa / Yesu (a.s), naamini darasa hili muhimu  Watanzania wanalihitajia leo kuivaa na kuiunga Mkono kwa hali na mali.

Dini zote zilizotoka kwa Mungu, Vitabu vyote vilivyotoka kwa Mungu,ikiwemo Taurati,ikiwemo Injiir, ikiwemo Zabour na ikiwemo Qur’an takatifu, vitabu vyote hiyo ukijaribu kivisoma kwa umakini vyote vimekuja kumuunganisha  Mwanadamu na wala sio kumgawanya Mwanadamu, Kama Mitume walifanya kazi za kuwaunganisha watu na vitabu vya mungu ukivisoma vyote vinakazi ya kuwaunganisha watu.

Hatuna kitabu cha Mungu kinachowagawanya watu,hatuna kitabu cha mungu kinachowabagua watu, hatuna kitabu cha mungu kinachowatenga watu, kwahivyo dini zote zilizotoka kwa mungu zote zimelingania kuwafanya watu kuwa kitu kimoja, 

zote zinawataka watu wasikilizane na waelewane, na mimi naamini na mtakubaliana na mimi watanzania wenzangu ya kwamba Moja ya mafunzo muhimu leo hii yanayotakikana kwa watanzania wote pamoja na tofauti za dini zao, wawe Waislam, wawe Wakristo, wawe Mayahudi na wawe wenye dini zingine zinazojulikana, naamini yakwamba mafunzo haya wanayahitajia Watanzania.

Na ninaamini vilevile taifa hili kwa darasa hili na somo hili linalofunzwa katika siku hii ya kumbukumbu ya kuzaliwa Muhammad (s.a.w.w) vilevile naamini Watanzania pamoja na Taifa kwa ujumla linahitajia.Bwana Mtume Muhammad (s.a.w.w) ameishi sehemu mbili huyu amabe tunamkumbuka leo hii kualiwa kwake, Bwana huyu ameishi katika mji wa Makka, ameishi vilevile katika mji wa Madina. 

Katika Mji wa Makka katika kazi alizozifanya nataka kuonyesha vipi Mtume alipokuwa Makka alijitahidi kuwaunganisha watu na si kuwagawanya.

Watu wa Makka au Wakazi wa Makka walikuwa na Dini tofauti, walikuwepo Wakristo, walikuwepo Mayahudi, walikuwepo wanaoabudu Masanam wanaoabudu Hubal, Lata Manata walikuwa ni waungu wao wakiwaabudu, lakini angalia Mtume Muhammad (s.a.w.w) alivyoishi na watu wa Makka, aliishi na watu wa makka mpaka wenyewe wakawa wanasema “Hatujawahi kukuona wewe ukiongopa katika jambo” huu ni ushuhuda au ushahidi unaotolewa na watu sio Waislam ndani ya ardhi ya Makka.

Hii ni kuonesha ya kwamba Mtume Muhammad (s.a.w.w) moja ya masomo yake muhimu yalikuwa ni kuwaunganisha watu, yaani kuunganisha Umma, yaani ni kuwafanya watu kuwa kitu kimoja na ilikuwa nikuwafanya watu waelewane, wasikilizane na wala sio kwenda kinyume na hivyo.

Wanamuambia Mtume (s.a.w.w) hatujawahi kukusikia wewe Ukiongopa,Historia inatuambia Mtume huyu tunaekumbuka leo kuzaliwa kwake, alikuwa akijulikana kwa siku mbili muhimu, sifa ya ukweli na sifa ya uaminifu, Sifa ya Ukweli na Uminifu Mtume (s.a.w.w) ndani ya nchi ya Makka aliitwa na Waislam na wasiokuwa Waislam, sio waislam tu walimpa sifa hiyo.

Waislam na wasiokuwa waislam kwanini, kwasababu Mtume (s.a.w.w) katika Mafunzo yake ya Makka ilikuwa Watu wa Makka wawe kitu kimoja, ilikuwa jamii ya Makka iwe wamoja, naamini masomo haya, mafundisho haya na mahubiri haya leo hii sisi katika taifa hili la Tanzania tunayahitajia kwa kiasi kikubwa.

Katika kuunganisha jamii ya Makka, watu wa Makka waislam na wasiokuwa waislam amana zao, fedha zao, vitu vyao vilikuwa vikiwekwa nyumbani kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w), kwa Ibara iliyokuwa nzuri nyumba ya Mtume ndio ilikuwa Benki ya Watu wa Makka, naamini ya kwamba ilikuwa umoja wa hali ya juu.

Umoja uliompelekea mtu anaeabudu sanam, mtu anaemuamini Nabii Issa / Yesu (a.s) kwamba ndio Mtume wake, mtu anaeamini Nabii Mussa (a.s) ndio Mtume wake na Taurati na Injiir ndio vitabu vyao lakini amana zake anaziweka nyumbani kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w).

Mtume Muhammad (s.a.w.w) katika kuwaunganisha watu kuwafanya kuwa Kitu kimoja alijitahidi kupambana na utumwa na kujaribu kuondoa utumwa  kwa hali na mali katika jamii, alijitahidi kuwaondoa wanaoitwa Watumwa, akajaribu kufunza mafunzo ambayo yataondoa Utumwa katika jamii ili watu wawe kitu kimoja.
Mtume akafunza kwamba kunyanganya  ni jambo halifai ambapo kwa kipindi hicho lilikuwa ni jambo la kawaida, utapeli ni jambo halifai, akafunza rushwa haifai, akafunza uharibifu haufai yote yalikuwa ni mafunzo yake, kwanini kwasababu yanalenga kuifanya umma, kuifanya jamii kuwa kitu kimoja.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) akajitahidi jambo moja muhimu naamini leo linahitajika mmno kujaribu kunyanyua heshima na hadhi ya Mwanamke, Mwanamke alikuwa akionekana ni mtu wa daraja la pili,mtume akainyanyua hadhi ya mwanamke, mtume akafundisha hakuna Mfumo Dume ndani ya Uislam, mtume akafunza yakwamba mwanamke anayohaki ya kurithi kama vile anavyorithi mwanaume, mtume akafunza yakwamba mwanamke ni mmoja katika wanafamilia.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) akafunza kuwa mwanamke anayohaki sawa kama vile mwanamume, mtume akafunza kuwa mwanamke anayohaki ya kumiliki kama vile anavyomiliki mwanaume, Mtume akafunza mwanamke anayohaki yakushiriki katika maamuzi, anayohaki ya kushiriki katika kupiga kura, anayohaki ya kuendesha gari lake. 

Haya ndio yalikuwa mafunzo ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) katika kuonesha na katika kuunganisha jamii.Na nizungumze jambo nzuri zaidi Mtume Muhammad (s.a.w.w) walikuwepo baadhi ya wanawake wakimtembelea akinyanyuka kwa sababu ya kwaheshimu wanawake hao, kwahivyo naamini ya kwamba mafunzo haya ya kuwaunganisha watu ya kuwafanya watu kuwa kitu kiomja na dhana ya mwanamke kama alivyoifundisha Mtume , naamimi ya kwamba ni funzo muhimu watanzania wote wanalihitajia.

Vilevile jambo nzuri la kupendeza Mtume Muhammad (s.a.w.w) akajaribu kutengeneza na sio tu kuunganisha watu Mtume alivuka zaidi ya hivyo, Mtume alivuka na akatengeneza udugu, yaani Mtume alitengeneza Umoja hakuishia hapo na akaingia kutengeneza udugu ikawa huyu ni ndugu wa huyu, Yule ni ndugu wa Yule yote kwa nini ni kuakikisha jamii yote inakuwa kitu kimoja.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) alipohama kwenda madina, alipofika madina akaendelea na kazi hiyo hiyo akajitahidi kuunganisha katika ya watu waliohama kutoka makka kwenda madina, akajitahidi kuwaunganisha hawa wawe kitu kimoja, Mtume Muhammad (s.a.w.w) alijitahidi kuunganisha kati ya Makabila mawili yaliyokuwepo madina, kabila la AUS NA AZRAJ akayaunganisha makabila hayo na kuhakikisha yanakuwa kitu kimoja, 

si hivyo tu Mtume alipofika Madina akatengeneza umoja wa watu wa Madina, umoja huo ulikuwa unawakusanya Wakristo, unawakusanya Mayahudi na unawakusanya Waislam.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) akatengeneza kamati ya amani ya kuwalinda watu wa Madina Waislam na Wasiokuwa Waislam, kamati ya kuwalinda Waislam, Wakristo, Mayahudi walioko katika ardhi ya Madina, Mtume Muhammad (s.a.w.w) akakaa meza moja na watu hawa anaotofautiana nao Kidini, Kifikra na Kimtazamo.

Kwa umuhimu wa kikao kile cha Amani na Maelewano na umoja kwa watu wa Madina ningependa kunukuu beti kama mbili au tatu katika vitabu vya kihistoria bakubaliano yanaandikwa kwa kusemwa “Haya ni makubaliano kutoka kwa Muhammad (s.a.w.w) Mtume wa Mungu baina ya Waumini na Waislam, kwa ibara nzuri Mtume (s.a.w.w) anawaita Mayahudi, anawaita Wakristo anawaita kwa jina la WAUMINI, 

kwahivyo makubaliano yake anasema ni kati ya Waumini na Waislam mpaka mwisho wa makubaliano.leo naamini mafunzo haya tunayahitajia, kwamba kumbe sisi tunaoamini Qu’an na wenzetu wanaoamini Injiir na wanaoamini Taurati na Zabuuri Mtume Muhammad (s.a.w.w) ambae leo tunakumbuka kuzaliwa kwake hawa anawaita WauminiAnasema tena 

“ Na hakika Mayahudi wa Bani Aufu, hawa mayahudi na wanaowafuata mayahudi yani Wakristo na wengineo hawa wote ni waumii ni umma mmoja ni jamii moja, wao wanadini yao na waislam wana dini yao, kama kuna mtu alifundisha kuheshimiana katika dini, kuheshimu dini za watu basi Mtume Muhammad (s.a.w.w) atakuwa mtu wa kwanza na atakuwa anaongoza,

Mtume pia anasema “Kati ya mayahudi na wakristo wote walioko madina wao akishambuliwa Mwislam lazima wanyanyuke kumsaidia mwislam na mwislam watakapompata yahudi, watakapompata Mkristo anashambuliwa wao ni lazima na wao wanyanyuke wamsaidie Mkristo,” huyu ndio Mtume tunaemkumbuka leo hii,mtume wa huruma, mtume wa maelewano.

Mtume anasema tena “ yeyote atakaeishi hapa Madina  awe Mwislam awe Mkristo awe Myahudi yupo katika amani haya ndio makubaliano ya Mtume ambae tunakumbuka kuzaliwa kwake na tunamsheherekea Mtume aliefunza  hivi.aliewaunganisha watu hivi,
Nikimalizia nisema neon moja nzuri kwamba mafunzo yake yote Mtume Muhammad (s.a.w.w) katika maisha yake yote yalikuwa yamegubikwa kwenye huruma,mtume alikuwa mtume wa huruma,

 akiwaonea huruma watu wa aina zote, kwa hivyo siku hii ya kuzaliwa mtume na siku hii ya Maulidi ya Mtume (s.a.w.w).Moja ya Mafunzo makubwa ya kujifunza ni sisi kama watanzania kupambika na huruma ya Mtume (s.a.w.w), yule unaetofautiana nae Kidini, Kirai na Kifikra umuonee huruma sio uwe na roho mbaya dhidi yake, yule ambae unamuona hayuko katika dini yangu yupo katika dini nyingine, wewe wajibu wako kwa kumfuata Mtume ni kumuonea huruma.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) hakufunza ukatili, Mtume hakufunza chinjachinja, mtume hakufunza kukunja uso, mtume hakufunza roho mbaya, yoyote anaekuambia mtume amefunza roho mbaya, mtume amefunza chinjachinja, mtume amefunza kukunja uso, huyo bado hajamuelewa Mtume Muhammad (s.a.w.w), Mwenyezimungu anasmea katika Qur’an kumuambia Mtume Muhammad (s.a.w.w)

 “wewe umekubalika kwa sababu ya huruma uliyokuwa nayo” ndio maana Waislam, Mayahudi na Wakristo walikuwa wakihifadhi amana zao nyumbani kwa Mtume.Katika mafunzo aliyofunza Mtume yalikuwa ni Mapenzi, ni mahaba , ni upendo, maelewano, masikilizano, kumpenda jirani yako ndicho mtume alichofunza, Mtume alifunza waislam kupendana wenyewe kwa wenyewe, Mtume alifunza Waislam kupendana na Wasiokuwa Waislam,

 mtume alifunza kuwapenda mafakiri, alifunza kuwapenda masikini, alifunza kuwapenda wajane, alifunza kuwapenda mayatima
Alifunza kuwapenda watu wanaoishi katika mazingira magumu, alifunza kuwapenda kila watu wenye aina yoyote ya matatizo, hayo ndio yalikuwa mafundisho yake katika maisha yake, Mtume alifunza kusaidiana, Mtume alifunza ukarimu, Mtume alifunza kuvumiliana hata kwa mtu mnaetofautina Kidini na kifikra.

Mtume anawaambia anawaambia waabudu Masanam “Nyie mnadini yenu,na mimi nina dini yangu” ndivyo mtume alivyofunza akatufundisha ya kwamba “Hakuna kulazimishwa mtu katika dini” yaani hakuna kumlazimisha mtu kuifuata dini, jambo la kufuata dini ni jambo la kukinaika na kuridhia kwa mtu mwenyewe binafsi, mafunzo haya leo yanahitajika.Mtume alifunza kuishi kwa usalama, kuishi pasina mivutano, kuishi pasina misuguano, haya ndio yalikuwa mafunzo yake. 

Mwisho ni wito wetu kwa Watanzania kwa siku hii ya kuzaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w), Kama mafunzo ya mtume yalikuwa ni huruma, siku hii ya kuzaliwa mtume tunatoa wito kwa watanzania wawe na tabia ya kuhurumiana, matajiri wawahurumie masikini, wenye nacho wawahurumie wasiokuwa nacho, wenye elimu wawahurumie wasiokuwa na elimu, wenye uwezo wawaahurumie wasiokuwa na uwezo.

Katika siku hii ya Maulidi moja ya ujumbe muhimu tuubebe ni upendo na maelewano aliyoyafunza Mtume Muhammad (s.a.w.w) tuondoke na somo la maelewano kama watanzania, tupendane,hakuna sababu ya sisi kubaguana kwa sababu mitume wetu wote walikuja kufunza maelewano, mitume wetu wote walikuja kufunza kusikilizana, mitume wetu wote walikuja kufunza kuvumiliana, mitume wetu wote walikuja kufunza mtu aipende nchi yake, mtu kuwapenda watu wake, 

kupenda nchi yako ni katika imani.Hayo ndio mafunzo yaliyofunzwa na Mtume Muhammad (s.a.w.w) na ninaamini ndio mafunzo  yaliyofunzwa na Nabii Issa / Yesu (a.s) na ndio mafunzo ya Nabii Mussa / Mosses (a.s), na ndio mafunzo ya Yohana na ndio mafunzo ya Mitume wote wa Mwenyezimungu (swt), katika siku hii ya Maulid turudi katika mambo hayo.

Mwisho niseme dini za mungu zimekuja kufunza amani, zimekuja kufunza utulivu, “Wewe mungu wewe ni amani” mungu mwenye anaeabudiwa na Waislam, anaeabudiwa na Wakristo, anaeabudiwa na Mayahudi, anaeabudiwa na Majusi mungu huyo anaitwa amani, “na wewe mungu kwako inatoka amani na kwako vilevile inarudi amani, “Mungu tufanye hapa Tanzania, na duniani kote tunaishi kwa amani.

Mitume wote wa Mwenyezimungu wamekuja kufunza amani, na Mungu tunakuwanae ni Mungu wa Amani, si Mungu wa Vita, si Mungu wa mivutano bali ni Mungu wa Amani na Masikilizano, Mungu tunakuomba utupe amani ya nchi yetu, Tanzania uzidi kuiboresha na kuifanya ni kisiwa cha amani na kisiwa cha masikilizano, uzidikuwafanya watanzania hawajui kubaguana kwa sababu ya dini zao, wabakie ni ndugu, 

wanasikilizana,wanaelewana, Mwenyezimungu tunakuomba vilevile Viongozi wan chi yetu, Utawala tuliokuwa nao Mungu uwape Hekima,busara, Utulivu waweze nao wawe ni chachu kuendeleza amani  tuliyokuwanayo, na watuongoze kwa busara na utulivu mpaka mwenyezimungu utakapoturudisha kwako.

Asanteni sana na hongereni Watanzania wote kwa kuzaliwa Kiongozi wa watu wote wa huruma, upendo na maelewano Mtume Muhammad (s.a.w.w).

Imetolewa Na:
Kiongozi Mkuu wa Waislam Dhehebu la Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala
10-12-2016, Jumamosi.

Sunday, December 4, 2016

“Waelezeni watu Uislam wa Mtume Muhammad (s.a.w.w) ni Uislam wa Huruma” Sheikh Jalala

Kiongozi Mkuu wa Waislam Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala akisisitiza jambo juu ya Uislam wa Mtume Muhammad (s.a.w.w) kuwa ni Uislamwa Huruma.
TAARIFA KWA UMMA WA KIISLAM
Sikuambii Huruma ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) kwa Waumini wa Kiislam mpaka akafikia mahala akasema “Yoyote mwenye kukiri Mungu ni Mmoja, mtu huyo ataingia peponi”hii ndio huruma ya Mtume (s.a.w.w) na Uislam aliotuletea.

Sasa ndugu yangu wewe unapata wapi fatua, unapata wapi Rai, unapata wapi Aya na Hadith za kumuambia mwenzako huyo ni Mtu wa Motoni wakati anasema Lailaha ilallah (Hakuna Mola apasaekuabudiwa ila Allah) Fatwa hiyo umeipata wapi?

Ni kwa mantiki gani unaetoa fatua ya kuuwawa Yule ambae unaetofautiana nae na yeye anasema Lailaha ilallah (Hakuna Mola apasaekuabudiwa ila Allah) Fatwa hiyo umeipata wapi?

Unapata ujasiri upi wa kuchukua mkono wako ukamuua mtu anaesema Lailaha ilallah (Hakuna Mola apasaekuabudiwa ila Allah)ujasiri  huo umeupata wapi?

Unatoa kwenye Qur’an gani fatua ya kuvaa bomo kwenda kulipua ndani ya Msikiti watu wanaosema Lailaha ilallah (Hakuna Mola apasaekuabudiwa ila Allah) Fatwa hiyo umeipata wapi?

Uislam wa Mtume Muhammad (s.a.w.w) bado haujulikani, Mnayo kazi ya kuwaeleza watu Uislam wa Mtume Muhammad (s.a.w.w) kuwa ni Uislam wa Huruma.

Imetolewa na
Kiongozi Mkuu wa Waislam Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala.
Ijumaa, 02-12-2016.



Thursday, December 1, 2016

KIFO CHA MTUME MUHAMMAD (S.A.W.W).

Tukio la kufishwa Mtume Muhammad (s.a.w.w) mbele ya jamii ni jambo geni sana, kana kwamba katika historia ya ulimwengu tukio hili halikutokea. Ingawa tukio la kuzaliwa kwa Mtume Muhammad limepokelewa kwa nafasi kubwa isiyo kifani. Kwa hiyo, unaweza kuona hafla mbalimbali za kusherehekea kumbukumbu ya kuzaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w) zikifanywa Misikitini, 

Madrasani, Majumbani, na katika Mazawia mbalimbali. Hili ni jambo jema sana, swali lilipo hapa ni, je, huyu afanyiwae haya yu hai mpaka sasa? Au amekwisha kufa? Ni kwamba Mtume Muhammad (s.a.w.w) amekwisha kufa. 

Sasa, tarehe ya wafat wa Mtume, Waislamu wanaichukuliaje. Inafaa ikumbukwe tarehe hiyo ya wafat tarehe ambayo Mtume Muhammad (s.a.w.w) ndiyo alioaga dunia, au haifai kuikumbuka?! Ilikuwaje! Maulamaa wa Kiislamu na Masheikh wa Twariqa katika tarehe zao za wafat hukumbukwa kwa visomo mbalimbali. 

Hili ni jambo jema, isipokuwa tarehe ya wafat wa Mtume Muhammad!!! Mtume (s.a.w.w) alipokaribia kufariki, kama ilivyopokewa na Ibn Abbas, alisema: “Nileteeni karatasi niwaandikie maandiko hamtapotea baada yake. Umar akasema Mtume anaweweseka. Katika riwaya nyingine, Umar akasema:

 “Hakika Mtume yamemzidi maradhi, na tunayo Qur’an inatutosha. Mara wakakhitilafiana (wako waliosema aletewe, na wako waliozuia) fujo likazidi. Mtume akawaambia: “Niondokeeni, na wala haipendezi kuzozana mbele yangu”.
Taz: Sahihi Bukhari:

Kitabul Itiswami bilkitabi wasunna, babu kara hiyatil khilafi.
Kitabul mardhaa, babu qawli quumuu anni.
Kitabun Nabi ila Kisra, babu maradhin Nabiyyi.
Kitabu Jihad, babu jawazil wafdi.
Kitabu IImi, babu kitabatil IImi.


Sahihi Muslim
Kitabul Waswiyya, babu tarkil waswiyya.

Kisha Mtume aliwaambia: “Niitieni Ali, Aisha akajibu: Laiti ungemwitisha Abubakar. Hafsa (naye) akasema: Laiti ungemwitisha Umar. (kila mmoja akawita baba yake) wakakusanyika mbele ya Mtume, Alipowaona Mtume akawambia: “Ondokeni nikikuhitajini nitakuiteni”.

Taz: Tarekhut Tabari J. 3 uk. 64
Mwana Aisha anasimulia kuwa: “Mtume alipougua maradhi aliyofia, aliamrisha Abubakar asalishe watu. Abubakar alipoingia Msikitini kutaka kusalisha, mara Mtume (s.a.w) akahisi woga, akatoka akiburuza miguu yake na huku ameshikiliwa na watu wawili (Ali na Abbas) alipoingia Msikitini, Abubakar akarudi nyuma ya safu, Mtume akakaa kuongoza swala.”

Taz: Tarekhut Tabari J. 3 uk. 64
Almuntadham J. 2 uk. 470


Katika riwaya hii, kuna mambo matatu yanahitaji kuangaliwa kwa kina:
Abubakar ni katika Maswahaba walioamriwa na Mtume kutoka pamoja na jeshi la Usama. Kwa hiyo, amma Abubakar alikwenda na jeshi kama Mtume alivyoamrisha, na kwa hiyo hakusalisha kwa sababu hakuwapo. Amma alikuwapo, kwa hiyo alipinga amri ya Mtume ya kwenda na jeshi, na kwa hiyo Abubakar amelaaniwa. 


Mtume (s.a.w.w) alipougua maradhi aliyofia: “Aitiwe Ali” tu, na wala si mtu mwingine. Na wapiga kampeni walipoita kila mmoja baba yake, Mtume aliwafukuza mbele yake, “ondokeni”. Mtume (s.a.w.w) amefariki akiwa kifuani kwa Ali bin Abi Talib ndani ya chumba cha Fatima (a.s). Anasema Imam Ali (a.s) kuwa: 

“Niliitwa na Mtume nikakaa naye karibu, nikampakata, akawa akininong’oneza kwa muda mrefu, mpaka mate ya Mtume yakanitiririkia!! Mtume (s.a.w.w) akakata roho akiwa kifuani kwangu!!!

Taz: Assiiratun Nabawiyya, ya Najahu Attai J. 2 uk. 316
At-Tabaqatul kubra J.2 uk. 26

Mtume (s.a.w.w) alivyotoka akichechemea taabani, na huku ameshikiliwa na watu wawili, Abubakar akapisha mahala hapo. Ni jambo gani lililomlazimisha Mtume kutoka akiwa hali hii, ikiwa yeye ndiye aliyeamuru kusalisha Abubakar? Ni kitu gani tena kilichomsonga kusalisha watu hali amekaa kwa taabu na dhiki kubwa? Kisha Mtume (s.a.w.w) akaagiza liandaliwe jeshi kupelekwa Rom. 

Mtume (s.a.w.w) akamteua Usama bin Zayd, kijana wa miaka kumi na saba au kumi na nane hivi aongoze jeshi hilo. Hii ni baada ya kumaliza hafla ya tukio kubwa lililotokea Ghadiir Khom ambapo Aya za Qur’an zilitemshwa, na Tamko la Mtume kutolewa na Waislamu wakatoa Baia yao kwa Imam Ali bin Abi Talib (a.s). 

 Mtume (s.a.w.w) akasisitiza Waislamu kujiandaa kutoka na jeshi hilo, akasema: “Andamaneni na jeshi la Usama, Mwenyezi Mungu amlaani atakaebaki nyuma”.
Taz: Afatu As-habil hadithi Uk. 12
Almilal wannihal J. 1 uk. 20


Katika Maswahaba walioamriwa na Mtume kutoka na jeshi la Usama ni Abubakar na Umar.
Taz: At- Tabaqatul kubra J. 2 uk. 190
Tarekhul Yaaquuby J. 2 uk. 113
Tarekh Ibn Athiir J. 2 uk. 215
Almuntadhan J.2 uk. 458


Kitendo cha Mtume (s.a.w.w) cha kumtawalisha Usama bin Zayd katika jeshi hilo, kilipingwa vikali na maswahaba: “Amemtawalisha kijana mdogo juu ya Muhajirina na Ansar wakubwa wakubwa!” Baadhi ya maswahaba walisikika wakipinga. Khabari hii ikamfikia Mtume, akawatokea akiwa amefunga kitambaa kichwani, kwa maumivu makali ya kichwa aliyokuwa nayo, akawaambia: 

“Japokuwa mnashutumu kutawalishwa kwake (Usama) bila shaka mlikwisha shutumu kutawalishwa baba yake zamani. Na kwa hakika. Usama anafaa sana kwa uongozi, na baba yake alifaa kwa uongozi huo. Basi jiandaeni kwenda (na jeshi la) Usama, Mwenyezi Mungu amlaani atakaebaki nyuma”. Usama akatoka pamoja na kikundi kidogo cha jeshi, akapiga kambi nje ya mji wa Madina mahala paitwapo Jurf.
Taz: Siiratul Mustafa Uk. 685-686
Tarekh Ibn Athiir J. 2 uk. 215
Tarekhut Tabari J. 3 uk. 54-55


Je, ni maswahaba gani waliopinga uteuzi wa Mtume? Vipi waandishi wengi wa Tarekh wamejiziwia kutaja majina yao? Miongoni mwa maswahaba waliopinga uteuzi wa Mtume ni Abubakar bin Abi Quhafa! Alikataa kwenda na jeshi la Usama, na badala yake akaenda kwa mkewe Habiba bint Khaarija aliyoko kijijini Sunhi, (nje kidogo ya mji wa Madina) hakurudi mpaka alipojulishwa kuwa Mtume amefariki!!
Taz; Tarekh Ibn Athii J. 2 uk. 218
Assaqiifa, ya Najahu Attaai Uk. 172-176


Mtume (s.a.w.w) amefariki tarehe 28 Swafar siku ya Jumatatu mwaka wa kumi Hijria. Familia ya Mtume ikakusanyika tayari kwa mipango ya maziko. Umar bin Khattb kuona hivyo, akachukua upanga akawa akizunguka huku na kule katika eneo la Msikiti na nyumba ya Mtume. Umar kwa sauti yake ya juu akawa anaonya: 

“Wanafiki wanasema Mtume amekufa, na hakika Mtume hakufa, atakaesema Mtume amekufa nitakata shingo yake”. Mpaka alipofika Abubakar akitokea kijijini kwake Sunhi kwa mkewe, akaingia ndani alipolazwa Mtume (s.a.w.w). Alipotoka akasoma Aya: “Na hakuwa Muhammad ila ni Mtume aliyepitiwa na Mtume kabla yake. Basi je, akifa au akiuliwa mtarudi nyuma kwa visigino vyenu? Na atakaerudi nyuma visigino vyake hatamdhuru kitu 

Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu atawalipa wanaoshukuru”. 3:144. Umar akasema: “Wallahi, kana kwamba watu hawajui kuwa Ayah ii ilishuka kwa Mtume”. Kisha Abubakar na Umar wakaondoka kwenda kwenye ukumbi wa Bani Saaidah kwa ajili ya uchaguzi.
Taz: Tarekh Ibn Athiir J. 2 uk. 219
Tarekhut Tabari J. 3 uk. 67-69
Nurul absaar Uk. 57-59


Kumbuka, Umar anasema: “Wanafiki wasema Mtume amekufa”. Je, ni nani wanafiki? Nyumbani kwa Mtume kuna: Ali bin Abi Talib, Fatima bint Muhammad, Abbas bin Abdil Muttalib, Alfadhl bin Abbas, Qutham bin Abbas, na Usama bin Zayd. (ilipotangazwa kuwa Mtume amefariki, Usama pamoja na kikundi chake cha jeshi walirudi mjini) Hawa ndiyo waliokuwamo nyumbani kwa Mtume pamoja na mwili wa Mtume, na ndiyo waliotangaza kifo cha Mtume. Kwa mtazamo wa Umar, hawa ndiyo wanafiki, na ndiyo aliokusudia kukata shingo zao!!

Abubakar na Umar hawakuhudhuria osho wala maziko ya Mtume, walikuwa kwenye ukumbi wa Bani Saaidah wakichaguana!!
Taz: Kanzul Ummal, kitabul khilafa maal-imaara khilafatu Abibakar
Almuswannaf, ya Ibn Shayba, babul Maghaz khilafatu Abibakar
Kama ambavyo, Mwana Aisha (mkewe Mtume) hakuhudhuria osho wala maziko ya Mtume, alipotea nyumbani kwa Mtume siku mbili, mwenyewe Mwana Aisha anasimulia hapa: “Wallahi hatukuelewa maziko ya Mtume mpaka tuliposikia kelele za majembe usiku wa Jumanne (wakati wakichimba kaburi):
Taz: Al-muntadham J. 2 uk. 482


Asiiratun Nabawiyya, ya Najah Attaai J. 2 uk. 314
Assunanul Kubra J. 3 uk. 574Tarekhut Tabari J. 3 uk. 81
Kifo cha Mtume kinatatanisha, je, amekufa kifo cha kawaida au ameuliwa kwa sumu? Anasema Mwana Aisha kuwa: “Tulimnywesha dawa Mtume wakati wa maradhi yake, na Mtume akiwazuia: “Msininyweshe”.

Taz: Tarekhut Tabari J. 3 uk. 62
Fat-hul Baary J.10 uk. 17


Waandishi wa kiislamu wanasema kuwa: “Waliohusika kumnywesha dawa hiyo kwa nguvu ni Aisha na Hafsa (wakeze Mtume) na kwamba dawa hiyo ni sumu!!
Taz: Assiiratun Nabawiyya, ya Najahu Attaai J. 2 uk. 379
Alburhan fyilafsiril Quran J. 2 uk. 117
Tafsirul ‘Ayyaashy J. 1 uk. 224
Tafsirus Saafy J. 1 uk. 389-390


Mtume (s.a.w.w) alikoshwa, kuswaliwa, kuzikwa na: Ali bin Abi Talib, Abbas bin Abdul Muttalib, Qutham bin Abbas, Alfadhlu bin Abbas, na Usama bin Zayd. Mtume (s.a.w) amezikwa siku ya Jumatatu, amepewa Utume siku ya Jumatatu, amehama Makka kwenda Madina siku ya Jumatatu, amefika Madina siku ya Jumatatu, na amefariki siku ya Jumatatu.
Taz: Almuntadham J. 2 uk. 477
Tarekhut Tabari J. 3 uk. 80

Imetolewa na:
Sheikh Rajabu Shaban Kabavako

MSAJILI WA HAZINA ATOA UFAFANUZI KUHUSU KUKAUKA FEDHA KATIKA MZUNGUKO, PAMOJA NA SABABU ZA MABENKI MENGI KULALAMIKA KUFILISIKA

 
Msajili  wa Hazina nchini, Lawrence Mafuru amesema benki nchini zinashindwa kueleza ukweli juu ya kuyumba kwao na kwamba madai ya kuwa hali zao ni mbaya kutokana na agizo la serikali la kutaka fedha zake zitunzwe Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hazina ukweli.

Mafuru amesema taarifa ambazo serikali wanazo ni kwamba benki hizo zaidi ya 50 zimekopesha fedha nyingi kwa watu mbalimbali, lakini marejesho ya madeni hayo yamekwama kiasi cha kusababisha benki hizo ziwe katika hali hiyo.

Akizungumza jana Dar es Salaam, Msajili wa Hazina licha ya kukiri kuwa mzunguko wa fedha umepungua kutokana na Tanzania kuchagua kwamba fedha inazozipata zitumike katika miradi ya maendeleo badala ya matumizi ya kawaida, benki zinazolalamika zimeshindwa kurejesha fedha ilizokopesha watu na taasisi mbalimbali.

Akizungumzia taarifa zinazoenezwa kwamba benki zimekosa fedha za kujiendesha, Mafuru alisema taarifa walizozipata ni kwamba Septemba mwaka huu, benki hizo zaidi ya 50 nchini zimekopesha zaidi ya Sh trilioni 16.3 kwa watu mbalimbali.

Hata hivyo, alisema kati ya fedha hizo, Sh trilioni 1.43 zimekopeshwa bila ya kurudishwa katika benki husika na kwamba benki hizo zinashindwa kueleza ukweli uliopo badala yake wanalalamika kwamba hatua ya serikali kuamua fedha zake zitunzwe BoT badala ya katika benki za kibiashara, ndio sababu ya hali yao (benki) mbaya.

Kwa mujibu wa Mafuru, serikali imeamua kuchukua uamuzi huo wa kuzitoa fedha zake kutoka katika benki mbalimbali za kibiashara nchini kwa ajili ya kuwezesha serikali kujua mapato wanayopata kutoka katika taasisi zake.

Msajili wa Hazina amesema zaidi ya Sh bilioni 515 zimeingizwa BoT baada ya uamuzi huo wa Serikali ya Awamu ya Tano ambao ulitangazwa na Rais John Magufuli baada ya kushika madaraka mwaka mmoja sasa. 

Mafuru alikiri kuwa ni kweli kwamba mzunguko wa fedha umekuwa mdogo na kueleza kuwa chanzo chake si kwamba benki zimekosa fedha kwa ajili ya kujiendesha.

Alifafanua kuwa awali watu wengi walitegemea safari na posho ambazo baada ya chenji kubaki, walikuwa wakitumia bila ya malengo, lakini sio kwamba mzunguko huo wa fedha unawaathiri watu wote.

“Tumeona tusitegemee wahisani badala yake tujiwekeze katika miradi mikubwa ya maendeleo ambayo kwa sasa haitaonekana, lakini baadaye itasaidia kuondoa nafasi iliyopo sasa,’’ alisema Mafuru.

“Tayari shilingi bilioni 515 zimeingizwa BoT na mpaka Septemba mwaka huu fedha hizo zilikuwa kwenye akaunti hiyo. BoT ni sehemu ya mfumo wa benki, kwani itakuwa inafanya kazi ya kukopesha kama zilivyo benki nyingine,” alifafanua Mafuru ambaye ofisi yake inasimamia mashirika na taasisi za umma.

Alifafanua kuwa ofisi yake ambayo ina jukumu la kusimamia mapato na matumizi, awali walikuwa wanapata shida kupata taarifa za mapato na matumizi katika benki hizo zilizopo kila kona nchini na kwamba baada ya BoT kuchukua dhamana hiyo, imewasaidia, kwani wanaandika barua na kupatiwa taarifa hizo kwa muda mfupi.

Alisema serikali inategemea mapato yake kutoka katika makundi matatu ambayo ni Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na kupitia mashirika na taasisi mbalimbali.

Alisisitiza kuwa itasaidia kujua mashirika hayo zaidi ya 260 namna wanavyotumia fedha zake katika miradi mbalimbali na kwamba suala la kuchukua fedha bila ya kuzitumia lisiwepo.

Wednesday, November 30, 2016

"Mtume Muhammad (s.a.w.w) umeweza kukaa na Wakristo, umeweza kukaa na Mayahudi,umeweza kukaa na Mapagani na umeweza kukaa na watu wa aina zote” Sheikh Jalala

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
MAADHIMISHO KIFO CHA MTUME MUHAMMAD (S.A.W.W) MWEZI 28, SAFAR 1438.

Napenda kuanza na mazungumzo yangu katika Qur’an Mungu ansema “Hatujakutuma ewe Muhammad (s.a.w.w) ila ni huruma kwa viumbe wote” siku hii ya leo ya mwezi 28,mfungo tano kwa kalenda ya Hijiria ndio siku ambayo Kiongozi wa watu wote duniani, kiongozi wa Waislam Mtume  wetu Muhammad (s.a.w.w) ndio ameaga dunia.

Weusi huu mnaouona, matembezi haya ya amani mnayoyaona yote ni kwasababu ya kukumbuka kifo cha mtukufu na mtakatifu Mtume Muhammad (s.a.w.w), Lakini lakujiuliza kubwa ni kwanini mtu huyu tumkumbuke katika kifo chake, zaidi ya miaka 1400 iliyopita. 

Sababu kubwa ya kukumbuka kifo cha Bwana Mtume Muhammad (s.a.w.w) kuna sababu nyingi mmno, lakini niseme sababu mbili tatu kwa harakaharaka, Sababu ya kwanza kama anavyosema Mwenyezimungu katika Qur’an kwamba “Wewe tumekutuma ukawe ni huruma kwa watu wote” sio huruma kwa Waislam, 


Sasa unapomuangalia Mtume Muhammad (s.a.w.w) wakati bado yupo hai, akiwa yuko katika mji wa makka na baada ya kuwa madina, tulimpata mtume alikuwa na huruma kwa watu wote, mtume alikuwa huruma kwa wasiokuwa waislam, mtume alikuwa na huruma kwa waislam, mtume alikuwa huruma kwa wtu waliokuwa wanaabudu masanamu, kwa watu waliokuwa wanaabudu lata, wanaabudu manata na wanaabudu hubal,

 hawa walikuwa ni waungu wakiabudiwa na warabu, lakini mtume aliishi vizuri na alikuwa ni huruma kwa watu hao, mpaka amana za watu hao aliziweka katika  nyumba yake,
Mtume alipokuwepo maka na madina vilevule alikuwa na huruma kwa Ahlulkitab / Wakristo, yaani alikuwa ni huruma kwa Wakristo, alikuwa na huruma kwa mayahudi na alikuwa ni huruma kwa watu wenye dini zote.

Naamimi ya kwamba huruma hii aliyokuwa nayo Mtume Muhammad (s.a.w.w) kabla hajaondoka duniani, naamini ya kwamba Watanzania na walimwengu huruma hii wanaihitajia.
Leo hii tunapotembea matembezi haya ya amani kwa ajili ya kukumbuka Mtume Muhammad (s.a.w.w) kifo chake, kubwa la kulienzi ni hili la Huruma ya Mtume Muhammad (s.a.w.w) inahitajika na ni muhimu, Naamini yakwamba Watanzania wote wanahitajia huruma aliyokuwa nayo mtume, huruma ambayo haikumfanya Mtume asiwapende wasiokuwa waislam.

Huruma ambayo ilimfanya mtume akae meza moja na Wakristo katika ardhi ya madina, Huruma ambayo ilimfanya Mtume akae meza moja na Mayahudi, huruma ambayo ilimfanya Mtume akae na Wakristo / Ahlulkitabu.

Naamini yakwamba leo hii Waislam watanzania Masheikh na Maimam na Maustadhi wanayonafazi kubwa yakumuenzi Mtume katika kukaa kwao na Wachungaji, wao na Maaskofu, wao na Mapari, wao na wenzi wao ambao wanatofautiana nao kidini, Naamini ya kwamba Matembezi haya yawe ni chachu yakuwafanya watanzania wote waiige huruma ya Mtume, 

ambayo huruma hiyo ilikuwa haimbagui mtu, huruma hii leo hii inahitajika mahala pakubwa.Bwana Mtume Muhammad (s.a.w.w) alikuwa ni huruma kwa watu wote kwanini kwasababu alikuwa na huruma na watu.

Jambo la pili Mtume ambae tunamkumbuka leo hii, ni mtume alieng’ang’ania na alieenzi Umoja kabla ya mtume hajaondoka makka alitengeneza umoja kati ya maswahaba wake, na alipoondoka makka kwenda madina vile vile akatengeneza umoja kati ya wakazi wa madina (Answar) na kati ya watu waliotoka Makka(Muhajirun).
Kiongozi Mkuu wa Waislam Dhehebu la Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala akiongea na Waandishi wa Habari katika Matembezi ya Amani ya Kuadhimisha Kumbukumbu ya Kifo cha Mtume Muhammad (s.a.w.w) Kigogo Round About, Leo Jijini Dar es salaam.Ambayo yalianzia Ilala Boma hai Uwanja wa Pipo Kigogo.

Akatengeneza Umoja kati ya makabila mawili yaliyokuwa yanavutana kabila la Ausi na Azraj, akatengeneza umoja wa Kidini ndani ya ardhi ya madina,naamimi ya kwamba leo hii, uwepo wa umoja wa Kidini ndani ya ardhi ya Tanzania,kipindi hiki ambacho huruma imekosekana , 

kipindi ambaho kuvumiliana kumekosekana, naamimi ya kwamba mafunzo haya Mtume Muhammad (s.a.w.w) yanahitajika leo hii kwa Watanzania na watu wote bila ya kuwabagua waislam wala wakristo wote wanahitajia umoja huu, wanahitajia kuishi huku kwa pamoja ameyoyafunza Mtume Muhammad (s.a.w.w).

Nimalizie kwa kusema yoyote ambae anafikra ya kwamba Uislam ni dini ambayo haina huruma huyo atakuwa hajautambua  Uislam, yoyote ambae anafikiria ya kwamba Mtume alikuwa ni mtu wa Misimamo ya kutisha ambayo hawezi kukaa na watu hayo hajamtambua Mtume. 

“Kwasababu ya huruma uliyokuwa nayo ewe Muhammad (s.a.w.w) watu wote wameweza kukukubali, umeweza kukaa na Wakristo, umeweza kukaa na Mayahudi,umeweza kukaa na Mapagani na umeweza kukaa na watu wa aina zote”

Jambo la Mwisho Mtume Muhammad (s.a.w.w) kama alivyoenzi Umoja, ulienzi utulivu, alienzi maelewano na alienzi amani, na ninaamini yakwamba Tanzania leo hii inayohaja kubwa yakuenzi Utulivu, yakuenzi Amani, yakuenzi Mshikamano watu kukaa pamoja, tofauti zetu za kifikra na za kimtazamo zisitufanye kutokuwa wamoja.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu wabariki wanadini wote walioko Tanzania, wabariki Viongozi wa Dini wahubiri Upendo, Maelewano, Mshikamano pamoja na Amani katika nchi hii,Vilevile Viongozi wetu na Serikali ambayo inatusimamia katika mambo yetu. 

Imetolewa na:
Kiongozi Mkuu wa Waislam Dhehebu la Shia Ithnasheriya Tanzania Sheikh Hemed Jalala
30-11-2016,Jumatano.